﻿Isaya.
54.
“Imba, ewe mwanamke tasa, wewe ambaye kamwe hukuzaa mtoto; paza sauti kwa kuimba, piga kelele kwa furaha, wewe ambaye kamwe hukupata uchungu; kwa sababu watoto wa mwanamke aliyeachwa ukiwa ni wengi kuliko wa mwanamke mwenye mume,” asema Mwenyezi Mungu. 
“Panua mahali pa hema lako, tandaza mapazia ya hema lako uyaeneze mbali, wala usiyazuie; ongeza urefu wa kamba zako, imarisha vigingi vyako. 
Kwa maana utaenea upande wa kuume na upande wa kushoto; wazao wako watayamiliki mataifa na kukaa katika miji yao iliyoachwa ukiwa. 
“Usiogope, wewe hutaaibika. Usiogope aibu, wewe hutaaibishwa. Wewe utasahau aibu ya ujana wako, wala hutakumbuka tena mashutumu ya ujane wako. 
Kwa maana Muumba wako ndiye mume wako, Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni ndilo jina lake, yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli ni Mkombozi wako, yeye anaitwa Mungu wa dunia yote. 
Mwenyezi Mungu atakuita urudi kana kwamba ulikuwa mke aliyeachwa na kuhuzunishwa rohoni; kama mke aliyeolewa bado angali kijana na kukataliwa,” asema Mungu wako. 
“Kwa kitambo kidogo nilikuacha, lakini kwa huruma nyingi nitakurudisha. 
Katika ukali wa hasira nilikuficha uso wangu kwa kitambo, lakini kwa fadhili za milele nitakuwa na huruma juu yako,” asema Mwenyezi Mungu Mkombozi wako. 
“Kwangu mimi jambo hili ni kama siku za Nuhu, nilipoapa kuwa maji ya Nuhu kamwe hayatafunika tena dunia. Hivyo sasa nimeapa sitawakasirikia ninyi, kamwe sitawakemea tena. 
Ijapotikisika milima, na vilima viondolewe, hata hivyo upendo wangu usiokoma kwenu hautatikisika, wala agano langu la amani halitaondolewa,” asema Mwenyezi Mungu, mwenye huruma juu yenu. 
“Ewe mji uliyeteswa, uliyepigwa kwa dhoruba na usiyetulizwa, nitakujenga kwa almasi, nitaweka misingi yako kwa yakuti samawi. 
Nitafanya minara yako ya akiki, malango yako kwa vito ving’aavyo, nazo kuta zako zote za vito vya thamani. 
Watoto wako wote watafundishwa na Mwenyezi Mungu, nayo amani ya watoto wako itakuwa kuu. 
Kwa haki utathibitika: Kuonewa kutakuwa mbali nawe; hutaogopa chochote. Hofu itakuwa mbali nawe; haitakukaribia wewe. 
Kama mtu yeyote akikushambulia, haitakuwa kwa ruhusa yangu; yeyote akushambuliaye atajisalimisha kwako. 
“Tazama, ni mimi niliyemuumba mhunzi, yeye afukutaye makaa kuwa moto, na kutengeneza silaha inayofaa kwa kazi yake. Tena ni mimi niliyemwambia mharibu kufanya uharibifu mwingi. 
Hakuna silaha itakayofanyizwa dhidi yako itakayofanikiwa, nawe utauthibitisha kuwa mwongo kila ulimi utakaokushtaki. Huu ndio urithi wa watumishi wa Mwenyezi Mungu na hii ndiyo haki yao inayotoka kwangu,” asema Mwenyezi Mungu. 
