﻿Zaburi.
146.
Msifuni Mwenyezi Mungu! Ee nafsi yangu, umsifu Mwenyezi Mungu, 
Nitamsifu Mwenyezi Mungu maisha yangu yote; nitamwimbia Mungu wangu sifa wakati wote ningali hai. 
Usiweke tumaini lako kwa wakuu, kwa wanadamu ambao hufa, ambao hawawezi kuokoa. 
Roho yao itokapo hurudi mavumbini, siku hiyo hiyo mipango yao yote hukoma. 
Heri yeye ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake, ambaye tumaini lake ni katika Mwenyezi Mungu, Mungu wake, 
Muumba wa mbingu na nchi, na bahari na vyote vilivyomo: Mwenyezi Mungu anayedumu kuwa mwaminifu milele na milele. 
Naye huwapatia haki waliodhulumiwa, na kuwapa wenye njaa chakula. Mwenyezi Mungu huwaweka wafungwa huru, 
Mwenyezi Mungu huwafumbua vipofu macho, Mwenyezi Mungu huwainua waliolemewa na mizigo yao, Mwenyezi Mungu huwapenda wenye haki. 
Mwenyezi Mungu huwalinda wageni na kuwategemeza yatima na wajane, lakini hupinga njia za waovu. 
Mwenyezi Mungu atamiliki milele, Mungu wako, ee Sayuni, kwa vizazi vyote. Msifuni Mwenyezi Mungu. 
